AFYA YA LWAKATARE NI MBAYA.....BADO ANASHIKILIWA NA POLISI


Dar es Salaam. Hali ya afya ya Mkuu wa Usalama na Ulinzi wa Chadema, Wilfred Lwakatare anayeshikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kuwahamasisha watu kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani kupitia mitandao ya jamii, imezorota.

Gazeti hili imemshududia jana akizungumza na wakili wake Nyaronyo Kicheere, huku akilalamikia hali yake kuwa si njema kutokana na ugonjwa wa kisukari alionao.

Alikuwa akitembea kwa kujivuta, na alidai kuwa ameshindwa kula chakula inavyotakiwa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, wakili Kicheere alisema amehangaika sana katika kuhakikisha kuwa mteja wake anapata dhamana lakini imeshindikana, hali ambayo inamtia hofu kutokana na hali aliyomwona nayo.

“Mteja wangu ni mgonjwa wa kisukari, kwa kawaida hutakiwa kula chakula na kunywa maji mengi, lakini nimehangaika sana, leo (jana) nilikuwa na matumaini kwamba atapelekwa mahakamani ambapo nilijipanga kwa kuandaa watu makini wenye hati za nyumba nikiwa na imani kwamba angepata dhamana, lakini wamemrudisha mahabusu,” alisema Kicheere.

Kicheere muda mwingi alionekana kuhaha kuwasiliana na viongozi wa Chadema kwa simu yake ya mkononi, pamoja na kuwasiliana na baadhi ya wanasheria akiwamo Tundu Lissu na Peter Kibatala ambao walijipanga katika kuhakikisha kuwa wanapata wadhamini watakaoweza kumdhamini Lwakatare.

Wakili huyo alisema kuwa kinachotendeka kwa mteja wake ni kinyume cha sheria kwa kuwa ni tuhuma ndizo zimemfanya akamatwe.

Alisema mteja wake ana haki ya kupewa dhamana hasa kwa kuzingatia kuwa saa zaidi ya 24 zimepita na hali yake si njema, na kwamba kuendelea kuwa mahabusu ni kuhatarisha usalama wa afya yake.

Posted by Bigie on 10:53 PM. Filed under . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0
.

Featured Post

NEC ya ahirisha uandikishaji kwa BVR mikoa 4 nchini

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeahirisha zoezi la uandikishaji kwa BVR katika mikoa minne  ambayo ni  Arusha, Kilimanjaro, Manyara pamoja ...

2010 BlogNews Magazine. All Rights Reserved. - Provided by Free Blogger template.