WOSIA WA "MZEE KIPARA" KWA WASANII WA TANZANIA ALIOUACHA SIKU CHACHE KABLA YA KIFO CHAKE


SIKU kumi zimekatika tangu kifo cha mkongwe wa uigizaji Bongo, Fundi Said ‘Mzee Kipara’, wapekuzi wetu wamenasa wosia wake mzito wa maneno aliouacha kwa mmoja wa mastaa wa sinema nchini.

Katika wosia huo, mastaa wa filamu za Bongo wametajwa huku pia wasiotajwa wakiguswa kwa namna moja au nyingine.

Staa huyo alisema, katika wosia huo marehemu alilalamikia tabia ya wasanii wenye majina, kwanza kuchukuana kimapenzi wao kwa wao, pili kutengeneza mabifu yasiyokuwa na maana  na tatu kushindwa kuheshimu kazi ya sanaa.

Akasema kwamba enzi hizo wakati wao wanafanya sanaa, waliiheshimu sana. Ilikuwa ni mwiko kwa wasanii kuchukuana wao kwa wao, labda kama kutakuwa na ndoa.

“Akasema  lakini siku hizi wasanii wamegeuza sanaa ni uwanja wa mapenzi bila heshima huku wengine wakinuniana.

“Aliwataja Ray na Kanumba kwamba walipokuwa Kaole hakuwahi kuwaona wamewekeana bifu lakini siku hizi wamepata majina makubwa, kila kukicha wanazuliana mambo.

Akasema, JB ni msanii wa siku nyingi sana, anashangaa kuona anakaa kimya mpaka wasanii wachanga kama Jacqueline Wolper na Irene Uwoya wanakwaruzana, Aunt  Ezekiel na Kanumba nao wanatibuana.

Pia mzee (Kipara) alisema Ray anatakiwa kuchagua mmoja katika mapenzi, kwa vile amekuwa akisikia yupo na Mainda, mara na Johari, ni vyema awe wazi kwa mmoja ili jamii ijue na kumheshimu kuliko ilivyo sasa,” alisema msanii huyo.

Aidha, alisema katika wosia wake huo, marehemu alikazia tabia ya mastaa, hasa wa kike kuacha kujirahisisha kwa wanaume kwani tabia hiyo inaondoa heshima yao na ya sanaa wanayoitumikia.

Akaongeza kuwa ni vizuri kama mastaa wa filamu wakajua umuhimu wa fani yao kwani siku zote inazingatia kuelimisha jamii kwa njia ya sinema, lakini kibao kimegeuka kwamba hata wao wanatakiwa kufanyiwa sinema za kuwaelimisha.


Katika maelezo yake, staa huyo alisema, wakati Mzee Kipara akizungumza hayo alionesha kutofurahishwa na tabia za baadhi ya wasanii ambao mara kwa mara wamekuwa wakiripotiwa kwa habari chafu.

“Hakufafanua zaidi kuhusu aibu wanayoweza kufa nayo wasanii wa filamu wasipobadilika lakini nadhani aliwataka wapendane, waache kutenda maovu na waiheshimu kazi yao,” alisema msanii huyo.

Katika maneno yake hayo mazito, staa huyo alimkariri marehemu akisema: “Kama hawatabadilika, mimi si nitakufa kifo nikiwa maskini, lakini wao watakuja kufa kifo cha aibu.”
 MZEE KIPARA WAKATI WA UHAI WAKE

Maneno hayo aliyoyatoa Mzee Kipara kabla ya kifo chake yanatakiwa kuwaingia wasanii wote kwani yanaweza kuwafanya wakaheshimika na hata watakapokufa wakaacha sifa nzuri nyuma yao.

Mzee Kipara alifariki dunia Januari 11, 2012 kwenye makazi yake, Kigogo jijini Dar es Salaam baada ya kusumbuliwa na matatizo ya miguu kwa muda mrefu.

Alizikwa kwenye makaburi ya Kigogo siku iliyofuata. Mungu ailaze mahali pema peponi roho yake. Amina.

Posted by Bigie on 10:38 PM. Filed under . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0
.

Featured Post

NEC ya ahirisha uandikishaji kwa BVR mikoa 4 nchini

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeahirisha zoezi la uandikishaji kwa BVR katika mikoa minne  ambayo ni  Arusha, Kilimanjaro, Manyara pamoja ...

2010 BlogNews Magazine. All Rights Reserved. - Provided by Free Blogger template.