CCM NA NCCR MAGEUZI WATOFAUTIANA UTEUZI WA MAWAZIRI

 
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) na NCCR-Mageuzi vimetofautiana kwa mtazamo kuhusu uteuzi wa mawaziri wapya uliofanywa na Rais Jakaya Kikwete.
 
Wakati CCM ikiunga mkono, NCCR imeponda uteuzi huo ikisema umeongeza mzigo kwa Serikali kwa sababu umeongeza idadi ya mawaziri na manaibu wao.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema uteuzi huo umezingatia mambo makuu matatu; Kilio cha Watanzania, watu wenye historia nzuri kwa utendaji na wasomi na ameweka sura mpya za vijana.

“Kwa kuzingatia kilio hicho, amewaondoa wale ambao walikuwa wanalalamikiwa,” alisema Nape.
Hata hivyo, Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi, Samuel Ruhuza, ‘ameponda’ Baraza la Mawaziri lililotangazwa jana na Rais Jakaya Kikwete na kwamba, limezidi kuwa kubwa tofauti na walivyotegemea.


Ruhuza alisema walitegemea Rais Kikwete angeunda Baraza dogo la  mawaziri ili kupunguza matumizi ya Serikali.
Alisema bado kuna tatizo la msingi katika uundaji wa Baraza la Mawaziri na kwamba, wanategemea ujio wa Katiba Mpya utaweza kutoa nafasi ya uundaji Baraza la Mawaziri kwa kuzingatia masilahi ya nchi.

“Katika uteuzi wa Baraza jipya la Mawaziri bado kuna tatizo, kwani tulitegemea lingekuwa la watu wachache ili kupunguza matumizi ya fedha za Serikali,” alisema Ruhuza na kuongeza:

“Tunategemea wananchi watatoa maoni yao juu ya suala la uundaji Baraza la Mawaziri kwenye ujio wa Katiba Mpya, ili kupunguza matatizo kama haya ambayo kwa sasa tunashuhudia tena leo yakijitokeza, badala ya kupunguzwa kwa wizara baraza hilo linaendelea kuwa kubwa.”

Ruhuza alisema hivi sasa imefikia wakati Tanzania kuiga mfumo wa Baraza la Mawaziri la Waingereza, kwani wao wana baraza la watu wasiozidi 20.
“Ni vyema na sisi tukaiga mifano wa nchi ambazo zimeendelea kama Waingereza, kwani wao wanapiga hatua za maendeleo kwa sababu ya  kuwa na baraza dogo la mawaziri lisiozidi watu 20,” alisema.

Chanzo: Mwananchi

Posted by Bigie on 3:41 AM. Filed under . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0
.

Featured Post

NEC ya ahirisha uandikishaji kwa BVR mikoa 4 nchini

Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeahirisha zoezi la uandikishaji kwa BVR katika mikoa minne  ambayo ni  Arusha, Kilimanjaro, Manyara pamoja ...

2010 BlogNews Magazine. All Rights Reserved. - Provided by Free Blogger template.