RAIS KIKWETE AWASILI MJINI ADDIS ABABA, ETHIOPIA KUSHIRIKI MKUTANO WA JUKWAA LA UCHUMI DUNIANI (WEF) KANDA YA AFRIKA
habari za kitaifa, JAMII 1:37 AM

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amewasili mjini Addis Ababa, Ethiopia usiku wa jana, Jumanne, Mei 8, 2012 kushiriki katika Mkutano wa Jukwaa la Uchumi Duniani (WEF) Kanda ya Afrika mwaka huu unaoanza kesho kwenye Hoteli ya Sheraton.
Mkutano huo wa siku tatu unahudhuriwa na mamia ya washiriki wakiwamo viongozi kutoka nchi saba zinazotekeleza mpango wa kilimo wa Grow Africa, sekta binafsi, wafanyabiashara, wasomi, wanazuoni na wanaharakati wa maendeleo ya Afrika.
Kabla ya kuanza rasmi kwa Mkutano huo mchana wa kesho, Rais Kikwete atakutana na viongozi wa mashirika yanayoshirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania katika juhudi kubwa za sasa za kuendeleza kilimo katika Tanzania kupitia mipango ya Kilimo Kwanza na Ukanda wa Maendeleo ya Kilimo wa Kusini mwa Tanzania - Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania (SACGOT).
Miongoni mwa viongozi ambao Rais Kikwete atakutana nao ni pamoja na Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID), Dkt. Rajiv Shah na Bwana Andrew Dell, Mtendaji Mkuu wa Benki ya HSBC-Africa.
Katika ujumbe wake mdogo, Rais Kikwete ameambatana na Mheshimiwa Profesa Jumanne Maghembe aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika hadi mabadiliko ya Baraza la Mawaziri wiki iliyopita na ambaye sasa ni Waziri wa Maji na Mheshimiwa Profesa Peter Msolwa, Mbunge wa Jimbo la Kilolo na ambaye alipata kuwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika.
Mbali na Rais Kikwete viongozi wengine ambao watashiriki katika WEF-Afrika mwaka huu ni Rais Paul Kagame wa Rwanda na Waziri Mkuu wa Ethiopia Meles Zenawi wakati nchi Ghana, Mozambique, Kenya na Burkina Faso zitawakilishwa na mawaziri.





